Serikali ya Uingereza imepitisha na kuzuia urushwaji wa ndege za bila ya rubani zenye uzito zaidi ya Gramu 250 bila ya kupata kibali maalum.
Hatua inakuja baada ya utafiti unaoonesha hatari ya kutokea kwa ajali za ndege na Helikopta.
Watumiaji sasa wa ndege hizo watalazimika kupewa majaribio kabla kujaza fomu maalumu ya kuruhusiwa kurusha ndege hizo.
Inaripotiwa ndege za bila ya Rubani 48 zilipotea nusu ya mwaka huu, na moja mwezi huu ilikaribia kusababisha ajali ya ndege baada ya kupita karibu mita 20 kutoka ndege ya abiria.
Ndege zisizo na rubani zinaweza kuharibu au kutatiza mawasiliano ya ndege kubwa au helikopta alisema mkuu wa chama cha Marubani BALPA, bwana Brian Strutton.
Mkuu huyo anaamini serikali itachukua hatua za haraka kabla ya msiba mkubwa kutokea wa ajali utakaosababishwa na ndege zisizo na Rubani.
Mwaka jana Polisi ilirekodi matukio 3,456 ya ajali za ndege za bila ya rubani ambapo ni mara 12 ya matukio yaliyoripotiwa mwaka 2014.
Ndege za bila ya Rubani zimekuwa zikisaidia sana shughuli za kulinda magereza, kuchunguza miundo mbinu ya usafiri kwa ajili ya ukarabati au kusaidia huduma za Polisi na moto za kuokoa au utafutaji wa wahalifu wanaojaribu kukimbia.
Pamoja na faida hizo na zingine pia zinaweza kutumiwa vibaya. Kwa sasa waendeshaji wa kampuni za kibiashara wametakiwa kutoa taarifa kwa wasimamizi wa zoezi hilo ili kupata ruhusa hiyo kuendelea na kazi zao.
Tanzania kupitia mamlaka ya Usafiri wa Anga, TCAA Julai 11, 2017 ilipiga marufuku kurusha ndege hizo bila ya kibali maalumu.