Baada ya wiki moja ya uvumi, Kampuni ya HMD Global imezindua simu janja mpya ya Nokia 2 ambayo inatarajiwa kuuzwa kwa bei nafuu zaidi ikiwa na ujazo mkubwa wa betri.
Simu hiyo imezinduliwa leo na imeanza kupatikana katika soko la India na masoko mengine itaanza kupatikana katikati ya mwezi Novemba mwaka huu.
Nokia 2 itakuwa simu janja ya Android yenye bei nafuu zaidi kutolewa kwa mwaka 2017. Inakadiriwa kuuzwa kiasi cha dola 99 za kimarekani|Tsh. 222,651. Toleo hili linakuja baada ya uzinduzi wa simu nyingine katika siku chache zilizopita ya Nokia 7.
Simu hii inaonekana imelenga wale watu ambao wana matumizi ya kawaida lakini inawezesha kukaa na chaji kwa muda wa siku mbili bila ya kuichaji.
Betri la Simu ya Nokia 2 itakuwa yenye ujazo wa 4100mAh. Uhifadhi wa ndani (Storage) ni ukubwa wa 8GB.
Kwa upande wa mfumo endeshi toleo la Nougat 7.1.1 lipo ndani ya simu hiyo. Wakati ukubwa wa kioo utakuwa inchi 5.0 pamoja na RAM ya ukubwa wa 1GB.
Kamera ya nyuma itakuwa na 8MP na kamera ya mbele itakuwa 5MP na kamera ya nyma ina MP 8. Aidha prosesa ni ya aina ya Qualcomm Snapdragon 212 na kwa upande wa mawasiliano ina mpaka 4G.
Kwa maoni ya wengi simu hii inaweza kuwa mkombozi kwa watu wenye kipato cha kawaida kuweza kumudu kumiliki simu janja. Kama ambavyo tuliweka taarifa ya utafiti wa kuendelea kupanda kwa bei ya simu janja taarifa ya ujio wa Nokia 2 kunaweza kupunguza maumivu kwa wenye kipato cha wastani.