Katika dunia ya sasa kila mmoja anajitahidi kumiliki simu janja, lakini rais wa Urusi Vladimir Putin ameweka wazi kwamba yeye binafsi hatumii simu janja.
Rais Putin mwenye umri wa miaka 65 na anayeongoza taifa la watu milioni 144 aliyasema hayo huko Siberia alipokutana na wanasayansi na kushangaa kila mtu mfukoni mwake kulikuwa na simu janja.
Alisema hana maslahi ya kujiunga na mitandao ya kijamii ya habari tofauti na mwenzake wa Marekani Donald Trump ambaye hutumia Twitter kama silaha yake binafsi ya kisiasa.
Rais Putin anaamini iwapo angekuwa anatumia simu janja basi simu hiyo ingeita kila mara. Pia, Rais Putin husoma dondoo za taaarifa rasmi tu kwenye mitandao ya kijamii ingawa yeye mwenyewe hajajiunga na mtandao wowote wa kijamii.
Mwaka jana alipokutana na watoto wa shule aliulizwa kama anatumia Instagram au mtandao wowote wa kijamii na alijibu kwamba binafsi hatumii na kwamba siku yake ya kazi ni ngumu na hukamilika mwishoni kabisa wa siku.