Baada ya kiu ya watumiaji wa WhatsApp kusubiri kipengele cha kuweza kufuta meseji uliyomtumia mtu, sasa rasmi kipengele hicho kimewezeshwa kwa watumiaji takribani wote duniani kote.
Kipengele hicho kitamuwezesha mtu kufuta meseji aliyotuma kwa rafiki yake au kwenye kundi (Group Whatsapp) pindi pale atakapoona kuna haja ya kufanya hivyo. Kipengele hiki kilikuwa tayari kimeanza kutumika kwa watumiaji wa WhatsApp Beta katika nchi mbalimbali duniani. Lakini sasa kimewezeshwa kwa watumiaji wote wa WhatsApp.
Pia kipengele hicho kitamuwezesha mtu kufuta meseji ndani ya kipindi cha dakika saba na si zaidi ya hapo. Ina maana kwamba hata kama ujumbe utakuwa umesomwa lakini bado utaweza kuufuta kwa uliyemtumia. Baada ya kuufuta ujumbe kwa uliyemtumia ima rafiki au kundi, utatoweka mara moja na ataona/wataona meseji iliyoandikwa kwamba This message was deleted.
Njia ya kufuta Meseji
Namna ya kufuta ni kuubonyeza kwa sekunde kadhaa ujumbe unaokusudia kuufuta na kisha utabonyeza kitufe cha alama ya delete ambacho kipo juu. Na kisha itatokea menu yenye meseji tatu. Moja inasema DELETE FOR ME, CANCEL na DELETE FOR EVERYONE. Ili ufute meseji kule ilipokwenda inabidi ubonyeze DELETE FOR EVERYONE. Hii ina maana utaifuta kwako na kule ulipoituma.
Na ukibonyeza DELETE FOR ME ni kwamba utaifuta upande wako tu na kule ulipoituma itabaki kama ilivyo. Kumbuka kama hujapata kipenegele hicho ni kiasi cha kufanya masasisho kwenye WhatsApp yako.