Kampuni ya huduma za mawasiliano nchini Kenya ya Safaricom imetangaza ongezeko la mapato yake kwa asilimia 14.3 baada ya kukatwa kodi sawa na shilingi bilioni 55.29 za Kenya katika kipindi cha mwaka mmoja hadi Machi 31 mwaka huu.
Mkurugenzi mkuu wa kampuni ya Safaricom, Bw. Bob Collymore alisema matokeo hayo yanatokana na mkakati wa kuboresha huduma na bidhaa kwa wateja wake unaoendelea kufanywa na kampuni yake siku hadi siku.
Licha ya chngamoto zilizojitokeza kwenye ushindani wa soko, Safaricom inayotoa huduma za kufanya miamala ya kifedha imeongeza wateja wapya milioni 2.1 wa M-PESA. Kwa mwaka 2017/18 pato la M-Pesa limeongezeka kwa 14.2% kufikia Ksh 62.9bn huku pato lililotokana na kununua vifurushi vya intaneti likiongezeka kwa 24% sawa na Ksh. 36.4bn.
Aidha, sehemu nyingine ya pato lake limechangiwa kwa asilimia 28 kutokana na kufanya miamala ya nje ya nchi.
Ongezeko hilo la pato kwa Safaricom ni furaha kwa wanahisa wake ambao waliomba wapewe mgao wa Ksh. 44.1bn kiwango kilichoongezeka kwa 13.5%. Kampuni kupata faida kubwa mwaka hadi mwaka ni ishara nzuri ya kukubalika kwa wateja wake.
Vyanzo: Business Daily, mitandao mbalimbali