Samsung Galaxy Book ni tableti-laptop mpya kutoka kampuni ya Samsung. Samsung Galaxy Book ni laptop ikiwa na keyboard lakini keyboard yake inaweza chomolewa na ukaweza kuitumia kama tableti.
Samsung Galaxy Book haiji na Android, bali inakuja na toleo la Windows 10. Hii si tableti ya matumizi ya kawaida, inawalenga zaidi watu wenye lengo la kutumia kwa ajili ya kufanyia kazi mbalimbali.
Galaxy Book itapatikana katika ukubwa wa aina mbili, kutakuwa na toleo la inchi 10.6 na jingine la inchi 12.
Sifa zake mbalimbali ni pamoja na zifuatazo;
- Yenye ukubwa wa inchi 12 inakuja na prosesa ya Intel Core i5, wakati ndogo yake inakuja na Intel Core m3.
- Keyboard mchomoko (yaani inayoweza kuchomolewa na kutenganisha na kompyuta kuu)
- Kioo (Display) mguso na hivyo unaweza kutumia kama tablet na pia kuna peni spesheli inakuja pamoja na kifaa chako (kama ile ya kwenye simu za Galaxy Note) – Stylus.
- Toleo la inchi 10.6 linakuja na display ya teknolojia ya TFT Full HD LCD (1920×1280) wakati toleo la inchi 12 linakuja na display ya AMOLED (2160×1440).
- Programu endeshaji: Windows 10
- Zote zinakuja na kamera ya Megapixel 13 na kwenye selfi unapata kamera ya megapixel 5
- Toleo la inchi 10.6 litakuja na RAM ya 4GB na utaweza chagua kati ya toleo la GB 64 SSD na la GB 128 SSD.
- Toleo la inchi 12 litakuwa na matoleo mawili pia, toleo lenye RAM ya GB 4 na diski uhifadhi wa GB 128 na pia kutakuwa na toleo lenye RAM ya GB 8 na diski uhifadhi wa GB 256.
- Matoleo yote yanakuja na uwezo wa kutumia memori kadi (Micro SD).
- Mfumo wa kuchaji ni wa kupitia USB-C, Galaxy Book ndogo inakuja pia na sehemu moja ya USB ya kawaida (USB 3.1) wakati kubwa inakuja na maeneo mawili ya USB.
Teknolojia iliyotumika kwenye keyboard yake inahakikisha keyboard hiyo inapata chaji mara moja ikiwa imechomekwa kwenye kompyuta kuu. Na pia haitumii teknolojia ya bluetooth ili kuweza kufanya kazi, kupitia mgusano wake na tableti kuu itaweza kuanza kufanya kazi mara moja.
Bei?
$1,200 na zaidi. Itakubidi uwe na zaidi ya Tsh Milioni 2.5 kuweza kumiliki.
Kwa kiasi kikubwa walengwa wa tableti hizi ni watu ambao bado huwa wanapenda kukamilisha kazi au majukumu mbalimbali kwa urahisi zaidi kwa kutumia kompyuta ndogo na zinazoweza geuzwa kuwa tableti kwa haraka.
Apple na iPad hali itakuwaje?
Tayari soko la tableti linaloongozwa sana na tableti kutoka Apple, yaani iPad linazidi kuporomoka, ila ujio wa tableti zinazotumia Windows 10 na zenye uwezo wa kugeuka haraka kuwa kompyuta kutokana na uwepo wa Keyboard umebadilisha kwa kiasi flani hali ya soko.
Tableti za namna hii zinawalenga zaidi watu wanaoziitaji kwa ajili ya kikazi zaidi kuliko soko lile lilokuwa limezoeleka ambalo ni la watu wanaoziitaji kwa ujali ya kuangalia na kusikiliza muziki, filamu na kucheza magemu.