Baada ya kuwa na uvumi kwa muda mrefu kwamba Kampuni ya simu ya Samsung Galaxy ina mpango wa kuunda simu itakayo kuwa ina kioo chenye kujikunja na kujikunjua, hatua hiyo sasa inaelekea kuwa kweli.
Uvumi huo umepata nguvu katika majukwaa ya teknolojia baada ya kuvuja kwa hati za kuthibitishwa majaribio ya Wi-Fi na Bluetooth kutoka Korean National Radio Research Agency (NRRA).
Inaonekana teknolojia ya Wi-fi ilithibitishwa mwezi April na Bluetooth mwezi August mwaka huu katika hati ya uthibitisho.
Model ya simu hiyo inaonekana katika hati hiyo ni SM-G888NO. Ingawa halikuonekana jina la simu husika lakini jina linalokisiwa ni Samsung Galaxy X ambayo inadhaniwa kuwa na kioo chenye kujikunja. Hata hivyo inaweza kuwa ni simu nyingine kabisa.
Wazo la kuwa na simu yenye kioo chenye kukunjuka kwa Samsung sio jipya. Mwaka 2009 picha hiyo hapo juu ilichukuliwa katika maonesho ya kimataifa ya Teknolojia ya CES (consumer electronics Show) na kuonesha kwamba Samsung wana mpango wa kutengeneza simu ya kwanza duniani yenye kioo cha kukunjuka yenye kutumia teknolojia ya AMOLED.
Mei 12 mwaka 2011 watafiti kutoka kampuni ya Samsung walisema wamedizaini kioo chenye kujikunja na kukunjuka. Walisema wamekifanyia majaribio na kwamba wamepata matokeo mazuri wa ufanyaji kazi wake.
Kwamba wamebaini mwanga wa kioo hicho utapungua kwa asilimia 6 baada ya kukunjwa na kukunjuliwa mara 100,000.
Pia Desemba mwaka 2013 Samsung walitoa video inayoonesha kifaa cha cha kioo chembamba sana kama karatasi kinachojikunja cha teknolojia ya AMELOD.
Katika video, kifaa hicho kinaonekana kama filamu nyembamba ya plastiki, lakini inafanya kazi kama Smartphone au kompyuta, ikiwa na icon za programu kadhaa zinazotumika katika simu.
Mapema mwaka 2016 zilitolewa taarifa kutoka vyanzo vya habari vya Korea Kusini kwamba Samsung wapo kwenye maandalizi ya kutengeneza simu mpya itakayoitwa Samsung Galaxy X.
Kwa mujibu wa ripoti hizo kwamba muonekano wa Galaxy X ungekuwa wa kama wa simu za kawaida, lakini pale itakapokunjuliwa itakuwa na muonekano mkubwa kama Tablet.
Lengo la Samsung Galaxy ni kuendelea kuwa na Kioo kikubwa zaidi lakini bila ya kumchosha mtumiaji kuwa na simu kubwa isiyoshikika mkononi. Hivyo wameona ni vyema kutengeneza simu itakayo kunjuka na kufungika.
Itakuwa ni uamuzi wa mtumiaji mwenyewe aidha kutumia simu ikiwa na katika muonekano wa kawaida au kuikunjua na kuwa mfano wa Tablet.
Wazo hili linaelezwa lilikuja hasa baada ya kuzindua simu ya Samsung Note Edge na baadae Samsung S6 Edge zilizokuwa na kioo kilichopinda (Curved screen).
Hata hivyo matarajio ya simu hiyo kuwa tayari kuzinduliwa ni kati ya mwaka 2018 au 2019.
Aidha wazo la ujio wa simu ya namna hiyo linaweza likawa la kupendeza na kusisimua lakini inaoneka wazi haitakuwa na bei nafuu.