Tangu kurudi kwenye ushindani Nokia wamekuwa wakitoa simu janja ambazo zinatokea kupendwa na wateja hivyo kuifanya kukubalika sokoni. Nokia 7.1 imezinduliwa rasmi baada ya vidokezo kadha wa kadha kuhusu sifa zake.
Tulishawahi kuleta vidokezo vichache kabisa kuhusu undani wa rununu Nokia 7.1 lakini simu hiyo imetambulishwa rasmi kwa ulimwengu na kiujumla imewekwa nguvu nyingi kuhakikisha kinachoonekana kwenye kioo kina ubora wa hali ya juu.
Undani wa simu janja Nokia 7.1.
Kipuri mama/Betri. Nokia 7.1 inatumia Snapdragon 636 SoC ambacho ni bidhaa ya Qualcomm yenye hadhi ya katikati. Betri la kwenye simu husika uwezo wake ni 3060mAh ikiwa na uwezo wa kuchaji haraka (kuchaji mpaka 50% ndani ya dakika 30). Pia inatumia teknolojia ya USB Type C.
Muonekano. Simu hiyo ina kioo kiitwacho Gorilla 3 chenye urefu wa inchi 5.84 ambacho kazi yake kubwa ni kuifanya kioo kutodhurika pindi simu itakapoanguka/kudondoka chini.
RAM/Diski uhifadhi. Simu hiyo inawezeshwa na aina tofauti tofauti za RAM/memori ya ndani; zipo zenye RAM GB 3 au 4, diski uhifadhi wa GB 32 au 64 GB lakini pia unaweza ukaweka memori ya ziada.
Kamera. Kwanza kabisa simu husika ina teknolojia ya HDR10 ambayo inafanya picha ziwe zitoke na mng’ao wa hali ya juu (1080 x 2280 pixel) lakini pia ikiwa na uwezo wa kubadilisha picha jongefu kutoka HDR kwenda SDR.
Kamera zake zipo mbili upande wa nyuma ambazo zina MP 12 nyingine ikiwa na MP 5. Kwa mbele ipo kamera moja tu ambayo ina MP 8 pamoja na kuwa na teknolojia ya kufunga/kufungua simu kwa kutumia jicho. Kubwa ambalo limenifurahisha ni uwezo wa kurekodi picha jongefu kupitia kamera zote kwa wakati mmoja.