Watoto watano wamefanyiwa upasuaji na kuwekewa vifaa maalum vya kusaidia kusikia (Cochlear Implant) jana wamewashiwa vifaa hivyo ili waweze kusikia kwa mara ya kwanza.
Zoezi hilo limefanywa na wataalam wa Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa kushirikiana na watalaam kutoka MEDEL .
Daktari Bingwa wa magonjwa ya Masikio, Pua na Koo Bw. Edwin Liyombo amesema Juni 5 na 6 mwaka huu watoto hao walifanyiwa upasuaji huo kwa mara ya kwanza na kuwekewa vifaa maalum kwa ajili ya kusikia (Internal complete) lakini jana wamekuja kuwekewa na kuwashiwa vifaa vya nje(External complete) ili waweze kusikia.
Kwa upande wake mtaalam wa vifaa vya usikivu Fayaz Jaffer amesema baada ya kuwekewa kifaa hivyo watoto hao wanapaswa kurudi kila baada ya wiki mbili kwa miezi mitatu na baada ya hapo watarudi wiki mbili kwa miezi sita ili kufanyiwa mazoezi.
‘’Baada ya hapo wanaanza kuwafanyia mazoezi ya kuongea (speech therapy) ndani ya mwaka mmoja na kadiri umri unavyozidi kwenda watakuwa wameshaanza kusikia na kujifunza kuongea na kupelekwa kujifunza zaidi katika shule za kawaida na si shule maalum kama ilivyozoeleka” amesema mtaalam huyo.
Juni 7 mwaka huu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mh. Ummy Mwalimu alizindua huduma ya upasuaji wa kupandikizaji wa vifaa vya usikivu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, ambapo katika Hospitali za Umma Tanzania imekuwa nchi ya kwanza kutoa huduma hiyo na ya pili katika nchi za Ukanda wa Afrika Mashariki ikitanguliwa na Kenya.
Cochlear Implant ni teknolojia ya kifaa cha umeme kinachofanya kazi ya kusaidia kusikia kwa sikio/masikio yaliyoharibika au kutokuwa na uwezo wa kusikia kabisa. Teknolojia hiyo huwekwa vifaa viwili, kimoja ndani ya sikio kwa njia ya Operesheni, na kingine huwekwa nje ya mwili kwa ajili ya kusaidia kutafsiri sauti.
Kifaa cha nje huvaliwa/kuwekwa nje ya mwili sehemu ya juu ya kichwa karibu na sikio la nje na huwa na Antena ndogo na Betri maalum inayowezesha mfumo mzima wa kusaidia kupatikana usikivu ambao awali haukuwepo.
kifaa hiki cha nje huchukua sauti za nje na kuzipeleka katika kifaa kilichowekwa katika sikio la ndani na kwa msaada wa ubongo hutafsiriwa na kuwa sauti. Teknolojia hii hutumika kwa ambaye amezaliwa masikio yote yamepoteza uwezo wa kusikia au sikio moja ama yule ambaye uwezo wa kusikia ni wa kiwango kidogo.