Utashi wa kutegemea kompyuta (uwezo wa kufikiri wa kompyuta) ama kwa lugha ya kigeni, Artificial Intelligence unaweza kuonekana kwenye matumizi ya kawaida kama Google Maps na magari yanayojiendesha lakini pengine hukujua kwamba watafiti mbalimbali wanangalia maeneo mengi ambapo unaweza kutumika kama kwenye kutabiri uamuzi wa mahakama.
Kwa mujibu wa tafiti mpya iliyochapwa na PeerJ Computer Science, ambayo inaundwa na Chuo Kikuu kinachoitwa University College London, Chuo Kikuu cha Sheffield na Chuo Kikuu cha Pennsylvania, utashi wa kutumia kompyuta umeonesha uwezo wa hali ya juu wa kutambua matokeo ya kesi za haki za binadamu kwenye Mahakama ya Kesi za Haki za Binadamu Ulaya – kwa asilimia 79!
Mbinu (Algorithm) iliyotumika huchunguza maneno (text) kwa machine learning – ambayo ni teknolojia zinazotumika kwa kompyuta kujifunza kutokana na data inayopewa. Waandishi wa mbinu hiyo hawatazamii ya kwamba utashi huu utatumika kama mbadala wa majaji na mawakili, bali unaweza kutumika kutambua tabia ya kesi flani flani na kesi gani zinapingana na makubaliano yahaki za Binadamu za Ulaya.
Utafiti huu wa PeerJ Computer Science umegundua ya kwamba maamuzi ya matokeo ya kesi za hapo mahakamani yanaridhiana sana na uhalisia na si moja-kwa-moja na sheria, hii ikiashiria ya kwamba majaji wanaangalia sana uhalisia wa jambo juu ya urasimu.
Hatahivyo, wachambuzi kadhaa wa sheria wameutazama utafiti huu na uwezekano wa kutumia utashi wa kompyuta mahakamani kwa mawazo tofauti, wakionesha wasiwasi wao juu ya “ethics” za kazi za mahakama – Si jambo jepesi kwa mashine kuamua kesi za binadamu.
Teknolojia hii inaangaliwa kwenye sehemu kadhaa zilizoendelea duniani, ikiwemo Korea ya Kusini, jimboni Florida Marekani kwa kuwa kuna ukweli kwamba teknolojia hii inaonesha uwezo mkubwa na kuna fursa ya kupunguza gharama za uendeshaji wa kesi.
Swali tunalokuachia nalo ni je, wewe unadhani ni sawa kutumia kompyuta kuamua kesi za binadamu hata kama zinaonesha uwezo mkubwa wa kuwa na uamuzi wa sawa na haki?
Chanzo: techRepublic