Kwa muda mrefu toleo la WhatsApp for Business, toleo rasmi la WhatsApp kwa ajili ya makampuni na biashara lilikuwa linapatikana na hakukuwa na mfumo wowote wa kuilipia huduma hiyo ila sasa maboresho kadhaa yanakuja pamoja na kuanzisha huduma zitakazohitaji malipo ili kuweza kuzitumia.
Tokea huduma ya WhatsApp kununuliwa na kampuni ya Facebook wengi waliamini muda si mrefu app hiyo itahusisha matangazo ya namna flani na pia wao kutafuta njia za kutengeneza mapato kupitia huduma hiyo. Facebook walilipa dola bilioni 19 kuinunua WhatsApp mwaka 2014 na sasa inaonekana muda wa kurudisha pesa hizo umefika 😀
Facebook wamesema wanaleta maboresho kadhaa kwa toleo la WhatsApp for Business, huduma zitakazo boresha uwezo wa biashara na makampuni kunufaika zaidi kwa kutumia huduma hiyo, ila pia makampuni hayo yajiandae kulipia baadhi ya huduma hizo.
- Biashara zitaweza kuuza bidhaa na kukamilisha mihamala ya pesa moja kwa moja kupitia WhatsApp, yaani mteja utaweza kuulizia bidhaa, kuichagua na kisha kukamilisha malipo bila kutoka kwenye app ya WhatsApp.
- Kutakuwa na huduma ya kuwezesha biashara kuwasiliana na wateja kwa urahisi zaidi kupitia tovuti spesheli itakayokuwa imeunganisha moja kwa moja na huduma ya WhatsApp. Kupitia tovuti hiyo biashara zitaweza kutunza vizuri taarifa za wateja wao, kufanya mawasiliano na kutuma jumbe kwa urahisi.
- WhatsApp for Business hadi sasa ina akaunti zaidi ya milioni 50
Facebook wamesema mabadiliko na maboresho hayo yanakuja muda si mrefu kuanzia sasa. Watumiaji wa WhatsApp for Business watakutana na maboresho hayo muda wowote kuanzia sasa.
No Comment! Be the first one.