Unakumbuka wakati wa ujio wa Halotel tuliandika uchambuzi mrefu tukieleza ni kwa namna gani tunategemea mtandao huo kuja kufanya vizuri? Kama uliikosa makala hiyo basi isome hapa -> Fahamu kwa nini mtandao mpya wa Viettel (Halotel) unaogopeka!
Kwa kiasi kikubwa tulikuwa sahihi, hili linaonekana kupitia data kadhaa ambazo zimekuwa zikitolewa na TCRA kila baada ya muda huku zikionesha mtandao huo ukizidi kukua kwa kupata wateja wapya huku kwa wakati huo huo mitandao mingine mikubwa ya simu ikioonekana ikidhidi kupoteza wateja.
Katika data za TCRA zilizooneshwa katika moja ya gazeti la kila siku siku chache zilizopita zinaonesha mtandao wa Halotel ukiongoza kwa ukuaji huku ukifuatiwa na Tigo huku mitandao mingine kama vile Airtel, Smart, Vidacom, TTCL na Zantel wote wakipoteza wateja katika kipindi cha kati ya mwezi Mei hadi Juni mwaka huu.
Data hizo zinaonesha mtandao wa Halotel uliongeza wateja 657,900 na huku Tigo ukioongeza wateja 383,117. Mitandao mingine imepoteza wateja, Airtel (-279,683), Vodacom (-193,627), Smart (-124,980), Zantel (-52,087) na TTCL (-98).
Ukichunguza kwa umakini data hizo utagundua ongezeko ni la wateja 390,542 tuu. Idadi nyingine yote ya nyongeza katika ongezeko la jumla ya wateja 1,041,017 limetoka kwenye wateja waliopotezwa na mitandao ya Airtel, Vodacom, Smart, Zantel na TTCL.
Data hizi ni za miezi ya tano na sita mwaka huu, picha ya data mpya zaidi zitatupa picha kubwa ya kuona ni jinsi gani ushindani kwenye sekta hii umekua zaidi.
Kumbuka katika kipindi cha miezi hii kadhaa tayari mitandao mingi inaendelea kuja na promosheni kubwa za kuvutia watumiaji. Mtandao wa Smart una moja ya vifurushi vya bei nafuu zaidi vya 4G unlimited kwa mwezi, kupoteza kwao watumiaji kunaweza kukawa ni changamoto inayosababishwa na 4G kukosekana kwenye miji mingine mikoani.
Je wewe unaonaje suala la ushindani wa huduma za mitandao ya simu? Je umebadilisha mtandao mwaka huu? Umeongeza upi? Umeukacha upi?
Kumbuka kusambaza makala na pia kuungana nasi kupitia Facebook, Twitter, Instagram, YouTube, Telegram na Google Plus
Chanzo: The Guardian