Shirika la Mawasiliano Tanzania TTCL limekanusha kuhusika na matatizo ya huduma za tiketi kwa mabasi ya mwendokasi (UDART) jijini Dar Es Salaam.
Kwa muda wa wiki sasa kumekuwa na matatizo katika ukatishaji tiketi wa mabasi ya mwendokasi ambapo imekuwa kero na usumbufu kwa wananchi wanaotumia huduma za mabasi ya mwendokasi.
TTCL kupitia taarifa iliyoitoa wiki hii imesema kwamba shirika hilo halihusiki na chochote zaidi ya kutoa huduma za mfumo wa mawasiliano kielektroniki (Internet Connectivity na Network Support) ambayo inatolewa kwa ufanisi mkubwa.
Taarifa hiyo imesema TTCL sio wahusika katika uuzaji na usimamiaji wa huduma za tiketi kwenye mabasi ya yanayotumia njia za mwendokasi kama baadhi ya watu wanavyodhani.
Aidha, TTCL imeongeza kusema haiwezi kuingia mkataba na UDART bila ya maridhiano na DART kama sheria na kanuni zinavyoelekeza.
Mwisho, taarifa hiyo imesema TTCL ni shirika la serikali kwahiyo mara zote itasimamia maslahi ya umma na wakati wote itaendelea kuweka mbele utoaji wa huduma bora kwa taifa.