Simu za HTC zina soko katika nchi nyingi tu na kuna watu ni wakereketwa wa simu kutoka kwa kampuni hiyo na huwa wapo karibu sana kufuatilia kuhusu toleo/simu janja ijayo kutoka HTC.
Kama ni mfuatiliaji wa simu rununu kutoka HTC utakuwa umesoma mahali kuhusu ujio wa HTC U12 Life lakini hukusoma kiundani sana. Sasa ukweli ni kwamba simu hiyo ipo njiani na sifa zake zimeshavuja.
Kipuri mama (processor). Huwa napenda kuanza kukichambua kipengele hiki kwa sababu katika kifaa chochote cha kidijitali kwenye kifaa hiki ndio kiungo kwa vitu vingine vingi (kama si vyote) iwe kwenye simu, kompyuta.
HTC U12 Life inaaminika kuwa itakuwa na moja ya kipuri chenye nguvu kiitwacho Qualcomm Snapdragon 636 SoC ambapo ni moja ya vipuri vyenye nguvu kutumiwa na makampuni mengi kwenye simu zao.
Muonekano/Kioo. Mabadiliko ya teknolojia yamefanya watu wengi kupenda simu ambazo zina kioo kipana na hata ukiishika mkono hakusumbui kwa hofu ya kuweza kuidondosha. Inaelezwa HTC U12 Life itakuwa na urefu wa inchi 6 (1080×2160 pixels) yenye teknolojia ya HD+.
Kamera. Karibu kila mtu ukimuuliza ni kitu gani simu janja nzuri iwe nacho hawezi kuacha kutaja kamera. Kwenye HTC U12 Life inaaminika kuwa na kamera mbili mbele zenye MP 16+MP 5 pia yenye uwezo wa kurekodi picha jongefu za ubora wa 4K huku kamera ya mbele ina MP 13.
RAM/Memori ya ndani. Makampuni mengi hivi sasa wakitoa simu ya hadhi ya kati basi kipengele cha RAM lazima kiwe kimeangaliwa kwa umakini, kwenye HC U12 Life utegemee GB 4 za upande wa RAM na GB 64 kwenye memori ya ndani.
Betri. Hakuna mtu anayeoenda simu yake iishiwe na chaji haraka na suala hili msingi wake huwa ni kwenye betri lenyewe lina nguvu kiasi gani. Kwa taarifa ni kwamba simu janja ya HTC U12 Life betri lake lina 3600mAh.
Kuhusu bei yake pengine haitakuwa chini ya $350|Tsh. 805,000 kwa kuagiza na ujio wa HTC U12 Life unategemewa ndani ya miezi michache ijayo.
Vyanzo: Gadgets 360, TechenGuru