Kama ulikuwa na mpango wa kununua simu mpya hivi karibuni? Kama una mapenzi ya dhati na simu zilizokwishajipatia umaarufu wa muda mrefu, za Nokia, basi unaweza subiri kidogo tuu.
Kampuni inayomiliki biashara za Nokia za simu kwa sasa, HMD Global, ya nchini Finland, imetoa taarifa rasmi wiki hii ya kwamba wameingia kwenye mkataba na kampuni mashuhuri ya matangazo ya biashara (marketing agency) ya ‘Mother’. Kampuni hii inafanya kazi tayari kutangaza bidhaa za makampuni mengine makubwa duniani kote, kama vile Coca-Cola.
Uamuzi huu ni moja ya maandalizi ya utambulishwaji rasmi wa simu za Nokia zinazotumia Android ifikapo mapema mwanzoni mwa mwaka 2017. Inategemewa ndani ya miezi 3 – 4 ya mwanzo wa mwaka simu za Nokia zinazotumia Android zitatambulishwa rasmi.
Hadi sasa habari za chini ya kapeti zinaonesha simu janja mbili za Nokia zitatambulisha mwanzoni mwa mwaka, na tutegemee kwa mwakani tuu simu za aina 2 – 4 zinaweza ingizwa sokoni.
Vyanzo mbalimbali za kutafuta habari za chini ya kapeti zinaonesha simu hizo zinasifa zifuatazo:
- Moja itakuwa ya ukubwa wa inchi 5.2, nyingine ukubwa wa inchi 5.5 (QHD Display)
- Programu endeshaji: Android 7.0 Nougat – toleo la kisasa kabisa la Android
- Prosesa – Snapdragon 820
- Kamera ya Megapixel 22.6
- Usalama dhidi ya kulowa na uchafu (dust & water resistant)
- Bodi la chuma (metal unibody)
- Kiwango kabisa cha betri bado hakijapatikana
Je wewe una historia gani na simu za Nokia? Je kama simu zitakuja kwa bei ya uhakika utafikiria kufanya maamuzi ya kununua?
Endelea kutembelea TeknoKona na tutakutaarifu mara moja tukipata habari zaidi kuhusu simu za Nokia.