Unapenda kuchomeka USB sticks (USB Flash) usizozifahamu vizuri kwenye vifaa vyako – (kompyuta, tableti, tv n.k)? Ukitumia USB Flash hii bahati mbaya itakuwa majanga.
Kifaa hichi kilichopewa jina la USB Killer ni kifaa kidogo kilichokama USB Flash ya aina yeyote ila chenye uwezo wa kuharibu kifaa chako chochote cha kielektroniki ndani ya sekunde-dakika.
Kitakapochomekwa kwenye kompyuta, laptop, tv, au kifaa chochote chenye mfumo wa USB kitanyonya kiasi kikubwa cha umeme kutoka kifaa husika, mfano kompyuta, na kisha kurudisha umeme huo kwa kiasi kikubwa – hali hii itafanya sehemu muhimu za kifaa husika kuungua kutokana na umeme mkubwa zaidi ya uwezo kurudishwa kwa wingi. Hali hii itaua kifaa husika kabisa.
Teknolojia hii imetokea wapi?
USB Killer imetengenezwa na timu ya watu wa masuala ya usalama (katika teknolojia za vifaa vya mawasiliano) ya jijini Hong Kong.
Timu hiyo ilishaongelea ukosefu wa usalama tosha wa teknolojia ya USB kwa baadhi ya vifaa na programu endeshaji, ila imeonekana makampuni mengi hayakuchukulia ushauri wao kwa umakini. Hadi ni sasa kifaa hichi cha USB Killer hakitafanya kazi kwa kompyuta za kisasa kutoka Apple tuu.
Ni Apple tuu ndio alichukulia ushauri wa timu hiyo ya utafiti kwa umakini na kufanya maboresho katika teknolojia ya USB kwenye vifaa vyake.
Kampuni inayotengeneza USB Killer imesema inategemea bidhaa yao itasaidia kuongeza ufahamu juu ya maboresho ya usalama yanayohitajika katika eneo la teknolojia ya USB.
Kwa sasa USB Killer inapatikana kwa takribani dola 56 za Kimarekani | takribani Tsh 120,000/=. Hatuwezi kuwa na uhakika juu ya upatikanaji wake nchini mwetu, ila tayari mtu yeyote kutoka mataifa mbalimbali anaweza agiza mtandaoni – https://www.usbkill.com/usb-killer/8-usb-killer.html