Kampuni ya Uchina ya Transsion Holdings inaongoza kwa mauzo ya simu za mkononi katika soko la Kenya kulingana na utafiti wa hivi karibuni.
Bidhaa zake tatu; Tecno, Infinix na itel ni miongoni bidhaa nyingine 5 za juu za simu zinazotumiwa na Wakenya nchini, kulingana na shirika la utafiti la Kenya la Consumer Insight.
Kwenye ripoti yake, simu janja hizo tatu zina jumla ya asilimia 54 ya simu zote zinazomilikiwa na wakenya. Mwaka 2016, bidhaa mbili za kampuni hiyo – Tecno na itel zilikuwa na asilimia 34 ya soko la simu nchini.
Kwa watu waliohojiwa katika utafiti huo, asilimia 28 wanatumia simu za Tecno, asilimia 16 simu za Samsung, asilimia 12 Nokia na asilimia 10 wanatumia Infinix.
Ripoti hiyo pia ilionyesha kuwa kampuni ya Transsion Holdings imechochea pakubwa kupanuka kwa utumizi wa simu za kisasa humu nchini. Kampuni hiyo kutoka Hong Kong ndiyo kubwa zaidi barani Afrika kwa mauzo.
Simu rununu nyingine kama vile Samsung (Korea Kusini), Huawei (China), LG (Korea Kusini) na Nokia zimepata ushindani mkali kutoka kwa simu janja za Uchina zinazoongoza kwa kuwa na bidhaa za bei nafuu kidogo ukilinganisha na sifa za simu husika.
Vyanzo: Daily Nation, Consumer Insight