Ndoa ni jambo la kheri na daima ni kitu ambacho kinakumbukwa lakini ikitokea muunganiko huo wa watu wawili (mke na mume) ukaingia dosari na hata kufikia hatua ya kutaka kutalakiana hapo kwa wengine simu inakuwa nyenzo muhimu.
Unaweza usiamini lakini ni vitu ambavyo vinatokea na badala ya kutumia kalamu na karatasi kuandika talaka au kutumia njia ya mahakama baadhi ya wanaume wameamua kutumia njia fupi; kutuma ujumbe mfupi wa maneno kwenda kwa mkewe kwa maana ya kwamba ndio talaka yake hiyo.
Labda Tanzania bara visa hivyo havijaibuka lakini kwa Tanzania Zanzibar mambo hayo yapo mpaka Waziri wa Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto kutoka SMZ, Bi. Moudline Castico kukemea na kupiga marufuku kwa wanaume kutumia njia hiyo kutoa talaka kwa mkewe.
Kitendo hicho (utoaji wa talaka kwa njia ya simu) kinatafsiriwa kama uzalilishaji na kumkosea heshima mwanamke hata kama haihitajiki tena kwa mumewe.
Bi. Castico alilisitiza kuwa taratibu statiki zifuatwe pale wawili hao wanapoona wameshindwana na kuachana kwa wema bila kumdhalilisha mwanamke.
Teknolojia ni nzuri lakini daima inatupasa tuitumie vyema kwa manufaa yetu. Simu kutumika kutoa talaka haina mantiki na inakiuka tamaduni zilizokuwepo miongo na miongo iliyopita. Tuige vitu vizuri lakini pia tudumishe tamaduni zetu.
Chanzo: Mtanzania