Malaysia imeripoti kuingia kwa virusi vya zika katika nchi hiyo baada ya mwanamke mmoja kupatikana na virusi hivyo, inasemekana kwamba mwanamke huyo alitembelea nchi ya Singapore hivi karibuni.
Waziri wa afya wa Malaysia amesema kwamba wanafanya jitihada za kuzuia maambukizi zaidi kwa kutokomeza mazalia ya mmbu katika mtaa aliokuwa anaishi mwanamke huyo, hatua hii inategemewa kuzuia maambukizi kusambaa zaidi.
Singapore ilitangaza kesi ya kwanza ya virusi hivyo vya Zika tarehe 27 mwezi Agosti na hadi leo tayari kuna kesi 115 ambazo zimeripotiwa na huku wathirika ni pamoja na raia wa nchi nyingine za Asia.
Virusi hivi ambavyo huambukizwa na mmbu vinahusishwa na microsefali ambayo husababisha watoto kuzaliwa na vichwa vidogo kuliko ilivyo kawaida, jina Zika ni jina la msitu huko nchini Uganda ambapo virusi hivi hiligundulika mara ya kwanza mwaka 1947.
Virusi hivi vinahusishwa zaidi na magonjwa kama dengue na homa ya manjano na hasa yanapatikana karibu na ikweta kati ya Afrika na Asia hata hivyo mwaka 2015 virusi hivi viligunduliwa katika nchi za bara la Amerika kusini na kusambaa mpaka visiwa vya Caribbean.
Kwa kuwa virusi hivi vinasambazwa na mmbu basi moja ya njia ya kujikinga navyo ni kutokomeza mazalia ya mmbu na pia kujikinga dhidi ya mashambulizi ya mmbu.