Uvamizi wa kutisha wa udukuzi wa mifumo ya kompyuta (Cyberattack) umeathiri maelfu ya mitandao katika nchi mbalimbali duniani, kwa kuingiliwa na virusi aina ya malware ambacho kinafunga mafaili ya kompyuta na kudai fidia.
Tishio hilo la udukuzi lilianza siku ya Ijumaa, wakati juhudi za uchunguzi bado hazikuzaa matunda katika kujua nani aliyeanzisha vita hii.
Uvamizi wa kutisha wa udukuzi huo wa mifumo ya kompyuta uliotokea siku ya ijumaa kwa muda kidogo na kushika kasi ya ajabu siku ya Jumamosi pia umezikumba nchi za Afrika.
Wataalamu wa usalama wa mifumo ya kompyuta wamewahakikishia watumiaji wa kompyuta ambao walikuwa wamehakikisha kuwa wamejadidisha (Update) mifumo ya “PC operating systems” watakuwa wamenusurika kwa kiasi fulani.
Wataalamu wameshauri kuwa wale wote ambao mitandao yao ilifungwa na kirusi kinachojulikana kama ‘ransomware’ wasifanye malipo yoyote waliotakiwa na wahalifu hao wa mitandao, ambazo ni Dola za Kimarekani 300.
Fedha hizo zinatakiwa kulipwa katika sarafu za kidigitali zijulikanazo kama bitcoin, mfumo ambao unapeleka fedha hizo katika kituo cha fedha kisichojulikana chenye herufi nyingi na nambari.
Hata hivyo watayarishaji wa kirusi hicho cha kidukuzi cha “WannaCry” ransomware chenye kufanya mashambulizi wamewaambia waathirika wake kiwango cha fedha kitaongezeka iwapo hawatofuata maelekezo katika siku tatu tangu udukuzi huo utokee.
Aidha wadukuzi hao wameonya kuwa iwapo watu hawatotii amri yao watafuta mafaili yote katika mfumo wa kompyuta hizo zilizoathirika iwapo malipo hayatofanyika katika kipindi cha siku saba.
Avast, ambayo ni kampuni inayotengeneza ‘software’ za ulinzi imedai kuwa inawatumiaji milioni 400 duniani, na imesema imebaini kirusi hicho cha ransomware kilichoshambulia, kiliongezeka kwa kasi siku ya Jumamosi kufikia dukuzi 57,000.
Avast ambayo iliasisiwa mwaka 1988 na watafiti wa Czech, imesema idadi kubwa ya udukuzi huo uliilenga Russia, Ukraine na Taiwan, lakini taasisi kubwa katika nchi nyingi duniani ziliathirika pia.
Wakati huo huo kampuni ya Microsoft imewatahadharisha watumiaji wake ku Update mifumo endeshi ya Kompyuta zao ili kujiweka katika mazingira salama dhidi ya udukuzi huo.
Msemaji wa Microsoft amesema hatua za kutoimarisha programu za mifumo endeshi mara kwa mara ndio sababu ya tatizo hilo.