YouTube Go ni app mpya kutoka Youtube inayolenga nchi zenye mtandao yenye uwezo mdogo na matumizi tofauti kama yalivyozoewa na nchi za magharibi ampabo Youtube imejipatia umaarufu na soko kubwa.
Mitandao yenye uwezo mdogo inatokana na soko kuwa dogo, yani watumiaji kuwa wachache. Kwa mfano India ina watu takribani bilioni 1.1 lakini kati ya wao, ni watu milioni 60 tu wanaotumia mtandao wa YouTube (Forbes). Dunia ya teknolojia inaziita nchi kama hizi kuwa za watumiaji “bilioni wanaokuja”.
Pamoja na India, nchi hizi ni kama Indonesia, Brazili, China na nchi za Afrika. Watumiaji hawa wanasemekana kuwa na mitandao tofauti, tabia tofauti za kijamii na mawazo tofauti kuhusu intaneti.
Kukabiliana na uwezo mdogo wa mtandao, Youtube Go inaminya na kutunza vipande vya video ili uweze kuangalia kilichopo. Unaweza kutafuta video, kuangalia video na kusambaza video bila ya kutumia mtandao wa simu.
Kwa kuwa kwenye nchi zetu gharama za kutumia intaneti ni kitu kinachotiliwa maanani sana, Youtube Go itakuonesha kiasi cha MB kinachotakiwa kutumika ili kuangalia video unayotaka ili uweze kuchagua kama uko tayari kutumia kiasi hiko kwa ajili ya video husika ili usimalize MB zako bila kujua.
Ukitaka kusambaza video kwa marafiki, YouTube Go itatafuta na kukuonesha watu walio karibu na wewe wanosubiria kupokea faili kupitia app hiyo.
Jambo ambalo linafanyika la kipekee kwenye YouTube Go na pengine la kuvutia kwa watengenezaji wa video ni kwamba wakati mtu unatuma video kwa mtu mwingine, app hiyo inafanya kazi ya kutoa taarifa ya kususha huko kwa mmiliki wa video ili awe na rekodi za kiasi gani video yake imesambaa. Jambo hili linafanyika kwa kutumia kiasi kidogo sana cha mtandao.
Kwa sasa Youtube Go inapatikana kwa watumiaji nchini India kwa kusajili hapa ila punde itakapo patikana kwengine, Teknokona itakujulisha wewe kwanza.
Kumbuka kusambaza makala na pia kuungana nasi kupitia Facebook, Twitter, Instagram, YouTube, Telegram na Google Plus
Chanzo: Wired.com, theVerge