Mahakama moja ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), imemhukumu mwanamke mmoja kifungo cha jela miezi mitatu kwa kupatikana na hatia ya kupekua simu ya mume wake bila ruhusa.
Mume wa mwanamke huyo alifungua mashtaka akimshutumu mkewe kwa kukiuka faragha yake na hivyo kujikuta akishitakiwa. Katika maelezo yaliyotolewa dhidi yake, mtu huyo alisema mke wake aliichukua simu yake na kunakili data zote katika simu nyengine ili kutafuta taarifa zake.
Aidha, mwanamke huyo alidai kuwa mume wake alimpatia nywila na kumruhusu kupekua simu yake tangu walipokuwa na ugomvi baada ya kukuta akiwasiliana na mwanamke mwengine.
UAE imeweka sheria kali za matumizi ya mitandao hususani katika suala la kulinda faragha za mtu mmoja mmoja mtandaoni. Mapema mwezi Agosti, rais Sheikh Khalifa alitangaza sheria mpya za matumizi ya mtandao ambapo atakaepatikana na hatia hukumu yake ni kifungo cha hadi miaka 25 jela.
Wanasheria Raed Al Awlaki na Mohammad Jad Al Mawla walieleza kwamba chini ya sheria za nchi hiyo, ni makosa kwa mtu yeyote kupekua simu ya mwengine bila ruhusa yake.