Kampuni ya usafirishaji ya Uber inawekeza dola za kimarekani milioni 500 katika mradi wake wa ramani hatua ambayo itapelekea kupunguza utegemezi wa kampuni hiyo katika mfumo wa Google maps.
Kwa sasa kampuni hiyo inayojiusisha na usafirishaji ulimwenguni inategemea Google map kwa kiasi kikubwa na katika maeneo mengi.
Uber inatoa usafiri kama wa taxi lakini ukiwa wa umeboreshwa kwa namna ambayo mteja anaweza kuita taxi na pia njia rahisi zaidi za kuweza kulipia huduma zilizotolewa. Mfumo huu unaifanya kampuni hii itegemee mfumo wa ramani wa uhakika saana, pengine hii ni sababu ambayo inawafanya Uber kuwekeza pesa nyingi katika mradi huu.
Japokuwa ramani kutoka Google Maps zinajitosheleza na zinataarifa nyingi za muhimu lakini wataalamu kutoka Uber wanasema kwamba taarifa nyingi katika Google Maps haziitajiki katika huduma za uber. Kinyume chake kampuni hii ya usafirishaji inahitaji taarifa nyingi ambazo Google maps haitoi, taarifa kama vile kuhusu foleni na maeneo ya kuwashushia ama kuwachukulia watu katika majengo hazipewi uzito na Google hivyo kutengeneza ramani zao kutasaidia kubadili tatizo.
Tayari kampuni hiyo ya usafirishaji imekwisha waajiri wataalamu wa mifumo ya ramani baadhi walikuwa wanafanya kazi katika kampuni ya Google, hii ni ishara kwamba hizi sio tetesi ila ni mpango ambao upo katika utekelezaji wake.