Siku hizi mawasiliano yamerahisishwa sana na sasa mtu anaweza akashinda siku nzima bila kuweka salio la kawaida ili aweze kupiga simu/kutuma ujumbe mfupi wa maneno kutokana na kwamba shughuli hiyo ameshaimaliza kupitia kifurushi cha intaneti.
Zipo programu tumishi kadha wa kadha amabazo zinatoa huduma ya kupiga simu/kutuma ujumbe mfupi wa maandishi kwa njia ya intaneti na moja ya programu hizo ni AIM (AOL Instant Messenger) ambayo kwa takribani miaka 20 imekuwa ikitoa huduma ya watu kuwasiliana kwa njia ya maandishi (SMS).
Historia fupi ya AIM (AOL Instant Messenger).
Programu hii wezeshi ya AIM ilianzishwa mwaka 1997 kwa lengo la kumuwezesha mtu kutuma na kupokea ujumbe mfupi wa maneno kwa msaada wa intaneti. AIM ni moja ya programu zilzowafundisha watu kujua namna ya kuwasiliana na watu kwa njia ya kuchati mtandaoni.
Ujio wa WhatsApp na Facebook Messenger ni moja ya sababu kuu zilizopelekea wamiliki wa programu wezeshi ya AIM kuifunga ifikapo Desemba, 15 2017 kutokana na kwamba progrgamu hiyo inatumiwa na watu wachache sana tofauti na miaka ya ’90 na 2000.
Ingawa programu hiyo itaacha kufanya kazi katikati ya mwezi Desemba ila haimaanishi kuwa barua pepe yako iliyo chini ya AIM (mfano@aim.com) haitafanya kazi tena la hasha! bali ni huduma ya kutuma na kupokea ujumbe wa maandishi tu ndio utafungwa ila barua pepe yako itaendelea kufanya kazi kama kawaida.
Kufungwa kwa AIM ni huzuni kubwa hasa kwa wale mpaka hivi leo bado wanaendelea kuitumia programu wezeshi ya AIM kuwasiliana na watu mbalimbali. Haina budi kukubaliana na hali na kuhamishia mapenzi yetu kwenye WhatsApp na Facebook Messenger.
Tuambie, wewe umeshawahi kutumia programu ya AIM? Habari hii ya kufungwa kwake itaathiri mwenendo wako wa kuwasiliana na rafiki/ndugu zako?
Vyanzo: TechCrunch, The Verge