Mwaka 2014 mwanzoni Tecno walitambulisha simu janja ambayo ilitokea kupendwa na hata hivi sasa naamini na watu bado wanapenda toleo hilo mpaka hivi leo ingawa kuna matoleo mengi tu ambayo yameshatoka.
Unaweza ukashangaa kwanini leo tumeamua kuichambua TECNO H5 ambayo ilitoka mwezi Februari mwaka 2014 lakini hii inatokana na ombi kutoka kwa mmoja wa wafuatiliaji wa makala zetu kutaka kuijua kiundani simu hiyo.
Tecno kama ilivyo makampuni mengine ya kuwa na tabia ya kutoa toleo jipya ambalo linakuwa linatoka kwenye familia moja kwa maana ya kwamba familia hizo zinaweza kuwa katika mfumo wa herufi au namba zinazofuatana na hapo ndio toleo la Tecno H5 lilipozaliwa baada ya mtangulizi wake Tecno H4.
Tecno H5 ina uwezo gani? (Sifa za Tecno H5).
Kioo/Muonekano. Simu ya Tecno H5 ni simu ambayo si nzito wala kubwa kwa muonekano; kioo chake kina ukubwa wa inchi 4 (wembamba wake ni 124 x 65.8 x 11.65mm). Ni simu janja ambayo hawezi kumkera mtu ikiwa mfukoni kutokana na uzito wake.
Programu endeshaji/Uwezo wa betri. Kwa mwaka 2014 roleo la Android 4.2.2 Jelly Bean ndio ulikuwa wakati wake na Tecno H5 ilikuja na toleo hilo hilo la programu endeshi la Android 4.2.2 Jelly Bean. Betri la kwenye simu ya Tecno H5 aina ya Li-Ion uwezo wake unaridhisha likiwa na nguvu kiasi cha 1800mAh; mtumiaji wa Tecno H5 anaweza kuongea kwa muda wa saa 5.33 (kwa matumizi ya kuongea tu).
Prosesa/Uwezo wa kamera. Prosesa ya kwenye simu hii ni dual-core CPU, MediaTek MT6572 chipset yenye kasi ya 1.0GHz. Kuna kamera mbili kwenye Tecno H5; kamera ya mbele ina MP 0.3 na kamera ya nyuma ina MP 5. Upande wa picha ya video ubora wake ni 720px.
RAM/Diski uhifadhi. Simu hii haina RAM kubwa ila kulingana na uwezo wa simu yenyewe MB 512 za RAM kwa mtu mwenye matumizi ya kawaida sana kwenye simu hii hawezi kuona Tecno H5 ni simu mbaya. Diski uhifadhi wa ndani peke yake ni GB 4 na pia ina uwezo wa kuweka diski uhifadhi wa nje wa mpaka GB 32.
Sifa nyinginezo. Inatumia laini 2 za simu, ina redio, kwenye masuala ya intaneti inakubali 2G/3G, bluetooth v3, inapatikana katika rangi nyeupe na nyeusi, inakubali WIFI hotspot, Wi-Fi direct na inatumia USB ndogo v2.0. Bei yake ni kati ya Tsh. 70 elfu-laki moja.
Tecno H5 ni simu kwa ajili ya matumizi ya kawaida na haishauriwi kuweka programu tumishi ambazo ni kubwa halafu ukazihifadhi kwenye memori ya simu; hii itafanya simu kuwa nzito na kupata moto haraka wakati inatumika (hasa intaneti ikiwa wazi).
Vyanzo: Oscar Mini, Best Mobs